nmb

nmb

Monday, April 15, 2013

SIMULIZI: ASIA DIGITALI SEHEMU YA 3


SIMULIZI: ASIA DIGITALI
MTUNZI: GEORGE IRON

SEHEMU YA TATU

*****
Juma akiwa katika kitanda hospitalini akiwa hoi kiafya analetewa taarifa ya kusikitisha lakini inayotia matumaini kidogo.
Gari lilikuwa limepatikana. Taarifa haikuishia hapo.
Gari lilikuwa ni sawa na kopo.
Tairi zote tano hadi ya spea, usukani, viti, taa, na redio havikuwepo tena.
Ilichekesha kuiita gari.
Jumanne akazimia tena.

****

Wakati Jumanne akiwa katika msihindano ya kuzimia na kuzinduka huku akifikiria maisha mapya bila kuwa na gari.
Wasichana watatu wenye maumbo ya tofauti lakini wakishabihiana rangi walikuwa katika meza mojawapo ya baa isiyokuwa maarufu sana katikaji ya jiji.
Walikuwa wameichafua meza kwa vinywaji mbalimbali huku nyama ya mbuzi ikiwafanyia tabasamu la dhihaka.
Walikuwa wameishughulikia na sasa ilikuwa imewakinai.
“Kwa hiyo hiyo laki mbili ya viti wanatoa lini.” Asia aliuliza baada ya kumeza funda la bia baria aina ya Kilimanjaro.
“Kesho jioni.” Mdada mnene kuliko wote aliyeathiriwa na utumiaji wa vipodozi vikali alijibu.
“Na yule bwege aliyechukua tairi mpya nd’o kasema anatuma kwa Mpesa au.”
“Kama kawaida yake.” Sasa alijibu Janeth.
“Kuhusu redio?” swali jingine kutoka kwa Asia.
“Ipo nyumbani kwao Messi”
Asia alimgeuzia macho yule dada aliyeathiriwa na vipodozi vikali.
“Husna Hakikisha huingii tamaa ukaiuza maana hukawii.” Asia alimwambia yule dada ambaye walimzoea kwa jina la Messi kutokana na mambo yake mengi.
Husna akatabasamu kisha akasema, “Nina dili jingine murua, redio kitu gani?” Husna alisema. Asia akapaliwa na donge la bia.
“Dili gani?” aliuliza kwa shauku.
Husna badala ya kutoa jibu, alizama katika mkoba akatoka na ‘business card’. Akamkabidhi Asia.
“Ya nini hii we Mmanyema.” Aliuliza.
“Chukua namba hizo.”
Asia hakuuliza swali, akaichukua namba.
“Nimekutana naye maeneo ya benki. Sho me me what u can do.”
Asia ahakujibu kitu. Alielewa Husna anamaanisha nini.
Janeth alikuwa amejikita katika kuzishambulia nyama huku Salome akiwa anafuatisha mashairi ya wimbo wa taarabu uliokuwa unapigwa katika baa hiyo.
Mavuno kwa siku hiyo yalikuwa mazuri sana.

*****

Dennis Kazinyingi alikuwa amejikita katika kutazama filamu ya kusisimua nyumbani kwake, mara uliingia ujumbe katika simu yake ya mkononi. Simu ilikuwa katika kiti kilichokuwa mbali naye.
“Neema….nipatie hiyo simu” alitoa amri.
Mtoto wake wa kike akaifuata na kumpatia.
Akaitazama namba iliyotuma ujumbe. Ilikuwa mpya.
Akaufungua ule ujumbe.
Kabla hajaanza kuusoma mara ikaingia simu.
Nayo ilikuwa namba mpya.
Akaipokea kwa utulivu wa hali ya juu.
“Halow…..Deniss Kazikwesha hapa.” Alijitambulisha kwa ujivuni wa hali ya juu.
“Samahani…aah shkamoo anko….sorry aaah nimekosea namba pliiz, nilikuwa namtumia mdogo wangu pesa nimetuma kwako.” Sauti ililibembeleza sikio la Dennis, hakika ilikuwa sauti ya kike isiyohitaji aina yoyote ya nakshi kuipendezesha.

“Pesa? Saa ngapi?”
“Sasa hivi, yaani muda si mrefu kaka yangu.”
“Ok ngoja nitazame nitakupigia.”
Simu ikakatwa, ujumbe uliokuwa unafunguka ulikuwa ujumbe unaoonyesha pesa imeingia.
Kutoka katika namba ile ile iliyompigia.
Shilingi laki mbili na nusu. Deniss akastaajabu kidogo, hakuingiwa na roho yoyote ya tamaa. Alikuwa ni mtu ambaye pesa kama ile si chochote kwake.
Akanyanyua simu yake akaipiga namba iliyompigia awali ikilalamika kukosea kutuma pesa.
“Wewe nd’o Asia?”
“Ni mimi kaka nisaidie tafadhali.”
“nipe dakika moja tafadhali.”
Simu ikakatwa tena. Kama alivyoahidi baada ya dakika moja alikuwa ametuma pesa kurudi kwa mmiliki.

“Game limeanza…..” ilikuwa sauti ya Asia akijisemea mwenyewe huku akimtazama Husna ambaye alikuwa amelala tayari.
Asia alijipongeza kwa karata ya pata potea aliyoweza kuicheza japo alikuwa na hofu ya kuibiwa ama kudhulumiwa kiasi hicho cha pesa.
Asia alikosea kutuma pesa maksudi, mwanzoni alitaka kutuma meseji na kujifanya kuwa amekosea namba, mbinu hiyo akaiona ya kianalojia sana.
Akataka kupiga na kujifanya amepiga bahati mbaya akaiona mbinu hiyo pia batili. Akaamua kuitumia mbinu ambayo matapeli wachache wanawewza kuitumia.
Akatuma kiasi hicho cha pesa.
Sasa pesa ilikuwa imerudi.
Asia akamshukuru Mungu wake, kisha akachukua simu yake akazipiga namba za Dennis, bila shaka jambo hilo hata Deniss alilingojea.
Nd’o maana akajitoa nje ya nyumba na kwenda katika bustani yake ndogo kuingoja simu ile.
“Ubarikiwe kaka yangu, yaani ubarikiwe sana, ni watu wachache sana wenye moyo kama wako, utaongezewa mara mia ya ulichonifanyia. Ujue ni ngumu sana kwa mtu ambaye hamfahamiani, ama kweli umenipa nafasi nyingine ya kuamini kuwa duniani bado kuna watu wana utu…..naomba nisizungumze mengi asante sana kaka yangu.” Alitiririka Asia, maneno kuntu lakini sauti mahaba,
“Usijali Asia, mambo madogo hayo nadhani huu ni mwanzo wa urafiki wetu, utajuaje maana ya Mungu mengi.’ Deniss alirusha kete yake.
“Haya Deniss mi nikutakie usiku mwema.”
“Haya asante japo hata sijajua unaishi wapi.”
“Mimi nipo Dar, sema ni mzaliwa wa Mwanza na mara kwa mara huwa nasafiri hapa na pale. Lakini kwa kifupi nipo Dar.” Alijibu.
“Ok mimi nipo Dar pia lakini nyumbani Maswa Shinyanga huko..ona sasa kumbe mimi na wewe wa kanda ya ziwa.”
Asia akatoa cheko la kisasa, cheko linalotangaza huba.
Walizungumza mengi. Usiku huu ukapita.
Asia akiwa hajamuuliza Deniss anafanya kazi gani. Hakutaka kupaparuka alitaka kushambulia taratibu lakini kwa umakini sana.

Siku iliyofuata, Asia akategemea kuwa Deniss atamuanza. Haikuwa hivyo.
Asia akajihisi kuchanganyikiwa kwani aliona dalili za kuupoteza ushindi zikimsogelea, na hakuwa tayari kukubali kushindwa ilhali alimuhakikishia Husna kuwa baada ya siku nne mambo yatakuwa sawa.
Asia akaamua kucheza pata potea nyingine.
Binti huyu aliyeemrejesha Jumanne kutoka katika kutembelea makalio mpaka kurejea mtaani kwa kutumia miguu, sasa alikuwa akicheza na namba nyingine asiyoifahamu.
Dennis. Anachokumbuka ni kwamba aliambiwa Deniss hana njaa na anaonekana ana pesa za kutosha.
Asia akisikia pesa, basi kuchanganyikiwa ni halali yake. Hakuna alichopenda kama pesa.

Asia akarusha kombora jingine.
Akaingia katika simu yake kitu cha kwanza akaandika ujumbe kisha akauhifadhi. Kitendo kilichofua akamtumia Deniss pesa kiasi cha elfu sitini za kitanzania. Kisha upesi akatuma ule ujumbe.
“Habari. Naomba upokee kiasi hicho kama shukrani zzangu za dhati kwa ukarimu ulionifanyia jana. Wewe ni wa ajabu sana. Ubarikiwe. Ninapotea hewani kwa dakika kadhaa naingia katika ndege naruka hapo Kampala mara moja. Nadhani kesho kutwa nitakuwa Dar. Take care.”
Kisha akazima simu yake.
Hakuna aliyeshirikishwa wakati mambo haya yanaendelea.

Deniss aliupokea ujumbe na pesa zile na kweli alivyojaribu kupiga namba haikuwa inapatikana.
Akaghafirika, hakutaka kushukuriwa kwa namna ile.
Alituma ujumbe lakini haukupokelewa na baadaye ulirejesha majibu kuwa haukufanikiwa kumfikia muhusika.
Deniss alikuwa katika mshangao wa hali ya juu, ujasiri wa Asia ulimshangaza. Hatimaye akapatwa na kile kitu ambacho Asia alikuwa anakijenga kwa kutumia gharama hizo.
Deniss akatamani kumuona huyu mwanadada ambaye kiuhalisia anaonyesha kuwa ni mjasiriamali haswaa.
Ni hicho Asia alikuwa anakihitaji.
Deniss na pesa zake zote alikuwa hajawahi kuipanda ndege, leo hii anatamkiwa na mtu kuwa ‘eti naruka hapo Kampala mara moja’.
Ni mtu wa aina gani huyu?
Akatamani kuiona sura ya Asia.

Baada ya siku mbili.
Asia alikuwa anapatikana tena.
Sauti ya ujivuni na majigambo ya Deniss haukuwepo tena kama awali, daraja alilokuwepo akamuweka na Asia hapo hapo.
Hata kumwambia kuhusua kuonana alikuwa anatetemeka. Lakini baada ya kumweleza Asia, alipata jibu jepesi lakini linalokera.
“Ngoja nicheki na ratiba zangu basi.”

Deniss alingoja kwa masaa mawili hatimaye akapokea ujumbe kutoka kwa Asia.
“Kesho saa moja hivi. Nitakuwa na kikao maeneo ya Hotel Valentine Kariakoo, na nitaimaliza siku katika hoteli hiyo kwani kuna mgeni wangu amefikia hapo. Karibu kama utaweza” Deniss akavuta pumzi. Akairudiua tena meseji ile. Hakika ilikuwa imetumwa na mwanamke jasiri sana, ambaye kukutana na watu ni jambo la kawaida sana.

Asia aliutuma ujumbe ule baada ya kufanya tathmini ya kina. Hakuhitaji kumchelewesha Deniss iwapo atajiweka machinjioni mapema.
Baada ya ujumbe ule alijitoa muhanga tena, akachukua chumba katika hoteli ile ambayo ina hadhi ya kuitwa hoteli. Hakuwa na kikao chochote bali alikua katika mawindo.
Alikuwa radhi kutumia pesa nyingi lakini mwisho wa siku apate nyingi zaidi, si kwa kuua mtu bali kuutumia mwili wake katika namna ya digitali.
Na katika dili hili hakutaka kuwashirikisha shoga zake wengine, hata Husna alitakiwa kungojea majibu tu.
SIKU ya siku ikafika, Asia kwa uvaaji wake hakika usingeweka tofauti yao na mfanyakazi yeyote katika benki ya dunia ama ikulu.

Siku iliyofuata majira ya saa moja jioni, Deniss alikuwa bize kubadili nguo, mara avae jeans.
“Ah hapa ataniona muhuni.”
Mara avae suti.
“Ah hapa nitaonekana mshamba sana….usiku huu na hili lisuti.”
Mara avae hiki mara kile.
Hatimaye akajituliza katika vazi la Jeans lakini juu akitua shati la mikono mirefu lililomkaa haswa.
Akaiendea gari yake na kuitia moto.
Safari ya kwenda kuonana na Asia.
Mtoto wa mjini.
Laiti kama angejua mtu anayekwenda kuonana naye.

**ASIA DIGITALI anaiseti chaneli mpya iweze kuwa halali yake…kumbuka ameshamgalagaza JUMA…….sasa anafanya shambulizi jingine.,…je DENISS naye anakamatika kiwepesi??

ITAENDELEA kesho hapa hapa

No comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

AddThis